JK: Hakuna atakayekufa kwa njaa

Na Mwandishi Wetu, Same. RAIS Jakaya Kikwete, ameuelekeza uongozi wa Mkoa wa Kilimanjaro na hasa Wilaya ya Same, kufanya tathmini kamili n... thumbnail 1 summary
Na Mwandishi Wetu, Same.
RAIS Jakaya Kikwete, ameuelekeza uongozi wa Mkoa wa Kilimanjaro na hasa Wilaya ya Same, kufanya tathmini kamili na ya haraka, kujua kiwango cha njaa katika wilaya hiyo, ili kuiwezesha Serikali kutoa chakula cha msaada ama cha bei nafuu kwa wananchi.

Aidha, Rais Kikwete amesema Serikali yake, itapata ufumbuzi wa kudumu juu ya changamoto ya maji katika maeneo ya Mkoa wa Kilimanjaro na hasa wilayani Same.


Rais Kikwete alitoa agizo la kushughulikia tatizo la njaa jana, wakati alipoelezwa na wananchi katika maeneo mbali mbali ya Wilaya ya Same, aliposimama mara kwa mara kusalimia wananchi kwenye siku ya pili ya ziara yake ya siku nne mkoani Kilimanajaro.

Wananchi katika maeneo ya Hedaru na Lembeni, walimwambia Rais Kikwete, kwamba wanakabiliwa na njaa kwa sababu ya ukame, ambao umesababisha wasipate chakula cha kutosha kwa miaka mitatu iliyopita.

Baada ya kusikiliza malalamiko hayo, hasa kuhusu njaa na ukosefu mkubwa wa maji, Rais Kikwete alisema,

“Nimesikia maelezo yenu kuhusu ukosefu wa chakula na njaa, Mkuu wa Mkoa yupo hapa pamoja na Mkuu wa Wilaya. Napenda kuwaagiza wafanye tathmini ya haraka, kuhusu kiwango cha tatizo, ili Serikali ichukue hatua ya kumaliza tatizo hili.

“Hakuna wasiwasi, hakuna mtu ambaye atapoteza maisha yake kwa sababu ya njaa, tunacho chakula cha kutosha na Serikali itahakikisha chakula kinapatikana mara tu tathmini itakapokamilika.

“Chakula kitakapoletwa kitakuwa cha aina mbili, kwa familia zisizokuwa na uwezo kabisa, chakula kitatolewa bure, kwa wale wanaojiweza, chakula kitatolewa kwa wananchi kuchangia fedha kidogo sana kama Sh 50 tu,” alisema Rais Kikwete.

Wakati wa ziara hiyo, Rais Kikwete alisimamishwa mara tisa na wananchi ambao walikuwa na hamu ya kumuona na kusalimiana naye, akiwa njiani kutoka Mamba Miamba, ambako alizindua Kiwanda cha Kusindika Tangawizi. Alikwenda Mwanga ambako alifungua Hosteli ya Shule ya Wasichana ya Asha Rose Migiro Mjini Mwanga.


Chanzo: Mtanzania