Na Mwandishi Wetu, Same.
RAIS Jakaya Kikwete, ameuelekeza uongozi wa Mkoa wa Kilimanjaro na hasa
Wilaya ya Same, kufanya tathmini kamili na ya haraka, kujua kiwango cha
njaa katika wilaya hiyo, ili kuiwezesha Serikali kutoa chakula cha
msaada ama cha bei nafuu kwa wananchi.
Aidha, Rais Kikwete amesema Serikali yake, itapata ufumbuzi wa
kudumu juu ya changamoto ya maji katika maeneo ya Mkoa wa Kilimanjaro na
hasa wilayani Same.
Rais Kikwete alitoa agizo la kushughulikia
tatizo la njaa jana, wakati alipoelezwa na wananchi katika maeneo mbali
mbali ya Wilaya ya Same, aliposimama mara kwa mara kusalimia wananchi
kwenye siku ya pili ya ziara yake ya siku nne mkoani Kilimanajaro.
Wananchi
katika maeneo ya Hedaru na Lembeni, walimwambia Rais Kikwete, kwamba
wanakabiliwa na njaa kwa sababu ya ukame, ambao umesababisha wasipate
chakula cha kutosha kwa miaka mitatu iliyopita.
Baada ya kusikiliza malalamiko hayo, hasa kuhusu njaa na ukosefu mkubwa wa maji, Rais Kikwete alisema,
“Nimesikia
maelezo yenu kuhusu ukosefu wa chakula na njaa, Mkuu wa Mkoa yupo hapa
pamoja na Mkuu wa Wilaya. Napenda kuwaagiza wafanye tathmini ya haraka,
kuhusu kiwango cha tatizo, ili Serikali ichukue hatua ya kumaliza tatizo
hili.
“Hakuna wasiwasi, hakuna mtu ambaye atapoteza maisha yake
kwa sababu ya njaa, tunacho chakula cha kutosha na Serikali itahakikisha
chakula kinapatikana mara tu tathmini itakapokamilika.
“Chakula
kitakapoletwa kitakuwa cha aina mbili, kwa familia zisizokuwa na uwezo
kabisa, chakula kitatolewa bure, kwa wale wanaojiweza, chakula
kitatolewa kwa wananchi kuchangia fedha kidogo sana kama Sh 50 tu,”
alisema Rais Kikwete.
Wakati wa ziara hiyo, Rais Kikwete
alisimamishwa mara tisa na wananchi ambao walikuwa na hamu ya kumuona na
kusalimiana naye, akiwa njiani kutoka Mamba Miamba, ambako alizindua
Kiwanda cha Kusindika Tangawizi. Alikwenda Mwanga ambako alifungua
Hosteli ya Shule ya Wasichana ya Asha Rose Migiro Mjini Mwanga.
Chanzo: Mtanzania