Kata tatu zaongoza kwa uchafu Ilala

Na Christina Gauluhanga, Dar es Salaam. KATA tatu za Manispaa ya Ilala jijini Dar es Salaam, zinaongoza kwa uchafu. Kutokana na hali hiyo,... thumbnail 1 summary
Na Christina Gauluhanga, Dar es Salaam.
KATA tatu za Manispaa ya Ilala jijini Dar es Salaam, zinaongoza kwa uchafu. Kutokana na hali hiyo, inawalazimu wasimamizi wa sekta ya afya, kuanzisha kampeni endelevu ya usafi ili kuepuka magonjwa ya mlipuko.

Akizungumza jana wakati wa kampeni endelevu ya usafi katika Kata ya Ilala ,Ofisa Afya, Idara ya Usafirishaji Manispaa ya Ilala, Charles Wambura, alisema kata hizo huzalisha tani 170 kwa siku.


Alizitija kata hizo kuwa ni Buguruni, Ilala na Vingunguti na kwamba, kwa sasa kuna mikakati iliyowekwa ili kutokomeza uchafu katika kata hizo.

Katika Kata ya Ilala, alisema wananchi huzalisha tani 35 kwa siku, Vingunguti tani 60 na Buguruni tani 75 hadi 80, huzalishwa kwa kuwa katika kata hiyo kuna soko kubwa.

"Tumeanza kuweka kambi katika kata hizo, kwa ajili ya kampeni endelevu ya usafi, ili kuepuka magonjwa ya milipuko.


“Lakini pia tumekumbana na changamoto mbalimbali, ikiwamo wananchi kushindwa kujitokeza katika usafi na kutokulipa ushuru wa taka," alisema Wambura.

Kwa upande wake, Ofisa Afya, Kata ya Ilala, Azizi Mkote, alisema wafanyabiashara 100 wa vipuri vya magari wameazimia kufanya usafi kila Ijumaa na Jumamosi, ili kuhamasisha suala la usafi wa mazingira.


Naye, Mkurugenzi wa Manispaa ya Ilala, Gabriel Fuime, alisema manispaa hiyo imesaini mkataba na wataalamu wa Serikali ya Ujerumani, ili kufanikisha ujenzi wa kituo cha kuchambua taka kinachojengwa eneo la Gongo la Mboto.


Fuime alisema kwamba, wametiliana saini mkataba huo na Kampuni ya Bremen Overseas Research and Development Associations (BORDA) na kazi rasmi ya kuchambua taka, itaanza Desemba mwaka huu baada ya ujenzi kukamilika.


Aliongeza kwamba, ujenzi wa kituo hicho ni mwendelezo wa kujenga vituo, kikiwamo kituo cha kuchambua taka kilichopo Vingunguti.

"Vituo hivi vitakuwa vinachambua taka, baada ya kukusanywa na wananchi. Lengo la kufanya hivyo kutaka taka zifikie zinakotakiwa kwenda zikiwa malighafi,” alisema Fuime.


Chanzo: Mtanzania