Na Mwandishi Wetu, Mpanda.
MWENYEKITI wa Shirika la Habari Njema kwa Wote, Askofu Charles Gadi,
amewaomba Watanzania na viongozi kubadilika kimawazo, kitabia na
kimatendo, katika kutunza mazingira, kwa ajili ya kunusuru wanyama walio
hatarini kutoweka kutokana na uharibifu wa mazingira na ukame.
Kauli hiyo aliitoa mjini hapa katika maombi maalumu yaliyofanyika
katika Mbuga ya Wanyama ya Katavi, ambako viboko wameanza kufa kutokana
na ukame.
Akitolea mfano wa viboko wanaotaabika na wengine kufa
kutokana na ukame, uliodumu kwa takriban miezi sita sasa, katika Mto
Katuma uliomo katika mbuga hiyo, Askofu Gadi, alisema kama mazingira ya
chanzo cha mto huo yangetunzwa vyema, wanyama hao wasingetaabika kiasi
cha kufa.
Alisema wakazi wa Katavi na Watanzania kwa ujumla,
wanapaswa kumcha Mungu, kwa kuwa hiyo ndiyo nguzo kuu ya kujitoa kwa
moyo wote katika kutunza mazingira na wanyama waliomo.
“Binadamu
ameacha kufanya mambo yanayompendeza Mungu, ndiyo maana haya yote
yanatokea, wakati umefika kwa kila mmoja wetu kuchukua hatua kunusuru
maisha ya viumbe hawa wasiyo na hatia,” alisema Askofu Gadi.
Kwa
upande wake, Mhifadhi Utalii, Costansia Maffa, alisema ukame unaondelea
hivi sasa katika mbuga hiyo umeathiri maisha ya wanyama wakiwamo viboko
na kuulazimu uongozi wa mbuga hiyo, kutumia njia mbadala za kuongeza
maji kwa kutumia mipira inayopita chini kwa chini katika Mto Katuma.
“Binadamu
hudhani kuwa wanyama ni adui, kumbe wanaweza kuwa msaada mkubwa sana
kwao, iwapo watapata ushirikiano na mazingira yao, kutunzwa vizuri.
“Kutokana
na ukame huu, maisha ya viumbe hawa kwa sasa yanategemea maombi yetu
sisi sote, kwa sababu hawa kama wanyama hawawezi kupiga magoti na
kumwomba msaada wa Mwenyezi Mungu, bali hilo ni jukumu letu binadamu,”
alisema Maffa.
Naye, Katibu wa Huduma wa Shirika hilo, Mchungaji
Palemo Massawe, aliwataka wahifadhi wa mbuga zote Tanzania kujiepusha na
vitendo vya kushirikiana na majangili kwa sababu kufanya hivyo ni
kulihujumu maendeleo ya Taifa.
“Hivi karibuni tumekuwa tukisikia
kutoka katika vyombo vya habari kuwa baadhi yenu mnashirikiana na
majangili kuwinda hawa wanyama, hii ni kinyume cha maadili ya kazi na
mafundisho ya Mungu,” alisema Mchungaji Massawe.
Awali akifungua
maombi hayo, Mkuu wa Mkoa wa Katavi, Dk. Rajabu Rutengwe, aliyataka
mashirika ya dini kuuombea mkoa huo mpya na rasilimali zilizomo uweze
kupiga hatua kubwa kimaendeleo.
Alisema hivi sasa mkoa huo
unakabiliwa na changamoto nyingi, zikiwamo za kijamii, afya, elimu na
miundombinu ya barabara na Serikali inajitahidi kuzitafutia ufumbuzi.
“Nawashukuru
waandaji wa mkutano huu. Maombi haya yatasaidia kuleta Baraka ya Mungu
na hatimaye mkoa wetu mpya, upige hatua kubwa za kimaendeleo kwa
haraka,” alisema Dk. Rutengwe.
Aidha, aliyataka mashirika mengine
kuiga mfano wa huduma njema kwa wote na kuongeza kuwa, kila mtu kwa
nafasi yake ni mdau wa maendeleo ya nchi.
Chanzo: Mtanzania