Nyumbu wanaozaa vitoto wavutia watalii 16,500

WATALII na watafiti 16,500 wa masuala ya wanyamapori kutoka mataifa mbalimbali duniani wamefurika katika Hifadhi ya Taifa Serenget... thumbnail 1 summary

WATALII na watafiti 16,500 wa masuala ya wanyamapori kutoka mataifa mbalimbali duniani wamefurika katika Hifadhi ya Taifa Serengeti, kushuhudia tukio la aina yake la nyumbu zaidi ya 8,000 kuzaliwa kwa siku, katika kipindi cha wiki sita.

Nyumbu hawa, wameanza kuzaliwa mapema mwezi huu na baada ya wiki sita wanatarajiwa kuzaliwa 500,000 lakini kati ya hao, karibu nusu yao, huliwa na wanyama wengine, wakiwapo simba, fisi na mamba kabla ya kukua huku wengine wakifa kutokana na kupotezana na wazazi wao.

Hifadhi hiyo yenye zaidi ya nyumbu 1.5 milioni, ina jumla ya simba 3,000 na fisi 7,500 ambao ndio walaji wakubwa wa nyama katika hifadhi hiyo.

Wakizungumza na waandishi wa habari, baadhi ya watalii hao, toka nchini Ubelgiji, Uingereza, Marekani na Ufaransa, walieleza kuvutiwa na tukio hilo, waliloliita kama “The Great Migration” .

Robert Joseph Raia wa Ubelgiji alisema, wamevutiwa sana na tukio la idadi kubwa ya nyumbu kuzaa kwa wakati mmoja.

“Ni tukio la ajabu duniani kila siku hapa nyumbu zaidi ya 8,000 wanazaliwa na watoto baada tu ya kuzaliwa dakika tano hadi nne,wanatembea”anasema.

Nicky Johnson raia wa Ufaransa, anaeleza kuwa, huu ni mwaka wake wa kwanza kufika Tanzania na Serengeti na alikuwa akiona kwenye mikanda ya video tukio la nyumbu zaidi ya 1.5 milioni kuhama na baadaye wakiwa Serengeti wanavyozaa na kuendelea na safari yao.
“Hili ni tukio zuri, sikuwahi kuliona sehemu yoyote duniani,hili ni jambo la ajabu , Tanzania mnapaswa kujivunia kwa tukio hili”alisema Jonson.

Mkuu wa Idara ya Utalii wa Hifadhi ya Taifa ya Serengeti, Godson Kimaro alisema tofauti na miaka ya nyuma mwaka huu kuanzia Februari Mosi hadi Februari 24, jumla ya watalii 10,621 toka nje ya nchi wamefika Serengeti kushuhudia nyumbu wakizaliwa.

Kimaro alisema katika kipindi hiki pia kuna Watanzania 5,815 wametembelea hifadhi, ikiwa pia ni ongezeko la zaidi ya asilimia 50 katika kipindi kingine.

Naye Meneja Uhusiano wa Shirika la Hifadhi za Taifa (Tanapa) Pascal Shelutete alisema Tanapa kuanzia mwaka jana, imeanza kulitangaza kimataifa tukio la nyumbu kuingia nchini, kuzaliana na kuondoka ili kuwavutia watalii.
Shelutete alitoa mwito kufika kuona maajabu hayo
Chanzo: Mwananchi

Una taarifa, picha za usafiri wa anga, mazingira, maliasili na utalii? tutumie kupitia kingkahindi@gmail.com