MCHANGO WA ZITTO WIZARA YA UTALII NA MALIASILI

Utafutaji haramu wa Uranium, Zitto ataka kauli ya Serikali. Saadani National Park na Serengeti International Airport zapigiwa chepuo. ... thumbnail 1 summary
Utafutaji haramu wa Uranium, Zitto ataka kauli ya Serikali.
Saadani National Park na Serengeti International Airport zapigiwa chepuo.

MHE. KABWE Z. ZITTO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Nitumie dakika hizi chache zilizobakia, kwanza napenda kuwapongeza wote upande wa Serikali na upande wa Upinzani kwa hotuba zao na ninaomba Serikali iweze kuzingatia maoni ya Kambi ya Upinzani na kuweza kuyafanyia kazi.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza ninaomba ufafanuzi nimeangalia ukurasa wa 60 wa Hotuba ya Bajeti kuhusiana na Halmashauri ambazo zimepatiwa fedha za mgawo wa uwindaji asilimia 25, Halmashauri ya Wilaya ya Kigoma haipo, na kuna mapori ya uwindaji. Huko nyuma tumekuwa tukipata mgawo kidogo. Naomba nipate maelezo ni kwanini katika kitabu cha Waziri hakuna mgawo huo wa Halmashauri ya Wilaya ya Kigoma.
Utafutaji haramu wa Uranium unaofanywa na kampuni ya Game Frontiers Ltd.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika hotuba ya Wizara ya Nishati na Madini, hotuba ya Wizara ya Ardhi na Maendeleo ya Makazi, na leo katika hotuba ya Wizara ya Maliasilina Utalii ya Kambi ya Upinzani tumezungumzia suala la mkataba wa kutafuta uranium kati ya kampuni ya Uranium Resources na kampuni ya Game Frontiers Ltd ambayo kwa njia zote imekiuka sheria ya madini ya mwaka 2010, sheria ya zamani ya madini ya mwaka 1997, Sheria ya Wanyamapori, Sheria ya Ardhi, na mpaka sasa hatujapata kauli rasmi ya Serikali kuhusiana na jambo hili. Tunaomba Serikali itoe kauli rasmi kuhusiana na kampuni binafsi iliyopewa kibali cha uwindaji lakini ikaingia mikataba kwa ajili ya utafutaji wa uranium.
Mheshimiwa Naibu Spika, jambo hili ni muhimu sana liweze kuchukuliwa hatua ili kuweza kuzuia na kuweza kuona kama kuna maeneo mengine ambapo jambo kama hili pia linafanyika. Naomba tuweze kupata kauli ya Serikali kuhusiana na kampuni ya Game Frontiers na kampuni ya Uranium Resources.
 Tulenge Watalii milioni mbili
[MHE. KABWE Z. ZITTO]
Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la Tatu; naomba kuzungumzia kuhusu potential ya utalii. Tunafahamu kwamba utalii  ndiyo sekta ambayo inaingiza fedha za kigeni ya pili baada ya madini. Lakini tofauti ya utalii na madini ni kwamba madini yanachimbwa yanapelekwa nje, utalii watu wanakuja wanaangalia, wanaondoka. Kwa hiyo utalii unabakia. Kwa hiyo hii ni resource ambayo inabakia. Kwa hiyo kuna kazi muhimu sana ambayo ni lazima watu tuifanye kwa ajili ya kuhakikisha kwamba utalii unaongeza fedha zaidi za kigeni. Mara kadhaa nimekuwa nikimwambia Waziri kwamba target yetu ya watalii milioni moja pamoja na kwamba hatujaifikia, lakini bado ni kidogo sana. Kwa potential tuliyonayo Tanzania, tunapaswa kuweka target katika miaka mitano inayokuja ya kufikia watafikia watalii milioni mbili na tunaweza tukaifikia iwapo tutarekebisha baadhi ya mambo fulani.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mfano, sasa hivi imeonekana kwamba Taifa ambalo utalii unakua sana kwa watu wanaotoka ni Russia, kwa hiyo ni lazima tujipange kama nchi, ikiwemo kuwa-train Watanzania lugha yao. Kuna Watanzania ambao wanajua hivi sasa Kirusi lakini tuwaandae vijana kwa ajili ya kuwa-train Kirusi kwa ajili ya kukuza utalii kutokea Russia. Lakini China Vilevile, Korea na India hizi ni nchi ambazo sasa hivi zinatoa watalii wengi sana. Kwa hiyo ni vizuri tuweze kujikita tuondoke katika idadi ya watalii laki nane na elfu sitini na saba ambao tunawapata hivi sasa tuende na target milioni mbili. Ninaamini kwamba tukifika huko tutakuwa tumepunguza sana tatizo letu la balance of payment kwa sababu sasa hivi mauzo yetu nje ni takribani dola bilioni sita tu, wakati manunuzi yetu nje ni tarkibani dola bilioni 11. Kwa hiyo utalii unaweza kutusaidia kuweza kuweka sawa urari wa kibiashara.
 [MHE. KABWE Z. ZITTO]
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini nina vitu viwili ambavyo nilikuwa napenda tuvitilie nguvu zaidi Bodi ya Utalii; Bodi ya Utalii inatangaza utalii nchi nzima. Kuna maeneo ambayo tuko disadvantage. Tuna hifadhi, tuna vivutio lakini matangazo yake siyo makubwa. Katavi National Park, Mahale National Park, Gombe National Park, na maeneo ya kale kama Livingstone ya Ujiji.
Mheshimiwa Naibu Spika, ni vizuri tuweze kuangalia namna ambavyo mamlaka nyingine ziweze kufanya matangazo yao, kwa mfano TANAPA. Hakuna sababu yeyote ya msingi kuwazuia TANAPA kuwa na Idara yao ya marketing ili wauze product zao kama TANAPA, ili kuweza kukuza maeneo mengine ambayo hatupati watalii kwa sababu tu ya matangazo na masuala mengine ya kimiundombinu ambayo naamini kwamba Wizara zingine zitaweza kuyashughulikia.
 Saadani NationalPark ipewe kipaumbele kikubwa
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kuna eneo very unique ambalo ni Saadani National Park. Ninapenda kuwashauri Wabunge wakipata muda, Saadani ni karibu sana na Dar es Salaam waende Saadani National Park. Hii ni hifadhi ambayo ikifanyiwa kazi vizuri Serengeti haitaona ndani. Kwa sababu ni hifadhi pekee ambayo maji chumvi na maji baridi yanakutana na yanakutana na bush. Bahari ya Hindi, mto Wami na hifadhi yenyewe ya Saadani.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo nilikuwa naomba tuifanyie matangazo maalum Sadaani. Saadani is very close to Dar Salaam, Sadaan is very close to Zanzibar, Sadaani is very close to Bagamoyo. Kwa hiyo, tunaweza tukaifanya Saadani kama project inayojitegemea kwa ajili ya kukuza utalii. Lakini pili hata utalii wa ndani tuweke utaratibu.
 [MHE. KABWE Z. ZITTO]
Mheshimiwa Naibu Spika, kuna reli inayopita Saadani kwenda Tanga, tuongee na watu wa Wizara ya Uchukuzi kuwe na weekend trains ambazo zinaenda Saadani kwa watu ambao wanataka kwenda over the weekends na kuongeza idadi ya watalii ambao wanapita pale Saadani.
Mheshimiwa Naibu Spika, ninaomba tufanye project maalum TANAPA na Wizara na Shirika la Reli kuhusu Saadani National Park. Ni hifadhi ambayo inakumbukumbu za asili, ni hifadhi ambayo imejaa historia, lakini pia ni hifadhi ambayo inaweza ikatuingizia mapato mengi sana ya kigeni.
 Serengeti International Airport, Mwanza.
Mheshimiwa Naibu Spika, jambo jingine ni Mwanza. Watu wengi sana wanadhani kwamba Arusha ndiyo njia ya kwenda Serengeti, Mwanza ni karibu zaidi na Serengeti kuliko sehemu nyingine yeyote ukiachana na Wilaya za karibu kama Serengeti na Bunda. Naomba tuwe na project maalum ya Airport ya Mwanza, na kuna kampeni ambayo sasa hivi inaendelea ya airport ya mwanza kuifanya kuwa ya Kimataifa na kuiita Serengeti International Airport. Tufanye kampeni maalum tuhusishe wadau wote na Airport ya Mwanza kama jinsi ambavyo tulivyojenga KIA kwa ajili ya utalii wa Kaskazini, tuijenge Serengeti International Airport Mwanza kwa ajili ya utalii wa Kanda ya Ziwa na utalii wa Magharibi ndege za kimataifa ziweze kutua, kwa ajili ya kukuza eneo hili kiutalii. Serengeti ni karibu zaidi na Mwanza kuliko Arusha ilivyo karibu na Mwanza.
 [MHE. KABWE Z. ZITTO]
Mheshimiwa Naibu Spika, tunafahamu kwamba ni lazima circuit ya Kaskazini kwa sababu ndiyo ambayo inatoa mapato mengi zaidi kwenye utalii kwa hivi sasa ni lazima tuiendeleze kwa sababu yenyewe ndiyo inatuzalishia fedha, lakini tutumie fedha hizo kukuza hayo maeneo mengine ambayo yanaweza yakatusaidia. Kwa hiyo ninaomba kampeni hii ya Serengeti International Airport Mwanza, iweze kukuzwa na tuweze kuiendeleza.
Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana ahsante sana.
 NAIBU SPIKA:
Waheshimiwa Wabunge, lakini kabla sijatoka hapa kwa nusu sekunde na mimi niseme kidogo. Jirani zetu ambao tunashindana nao mara nyingi wa Kenya, asilimia sitini ya utalii wao ni utalii wa Pwani ambapo ni maeneo ya Mombasa Lamu na Malindi. Wanategemea Marine, National Parks na Marine Reserves. Sisi Marine Reserves na National Parks zetu tulizo nazo zipo chini ya Wizara ya Wizara ya Mifugo na Uvuvi. Jana tulikuwa na Wizara ya Mifugo na Uvuvi ni nani aliongelea habari ya Utalii jana? Hivi ni kwanini Marine Parks na Reserves zisihamie Wizara ya Maliasili na Utalii?
 Kutamba kote kwa Kenya kunategemea Marine Parks and Reserves na sisi tuna Marine Parks and Reserves bora kabisa kuliko Kenya by far.
Kwa hiyo, naomba tupange mambo yetu vizuri, tukiwakabidhi Marine Parks and Reserves, TANAPA au Wizara ya maliasili na Utalii nina uhakika tunaweza tuka-double idadi ya watalii wetu kwa haraka sana.