Uchumi wa Tanzania unazidi kukua

Na Mwandishi wetu Uchumi wa Tanzania unaendelea kukua kwa kiwango kizuri cha zaidi ya asilimia sita tangu mwaka jana,... thumbnail 1 summary
Uchumi wa Tanzania unaendelea kukua kwa kiwango kizuri cha zaidi ya asilimia sita tangu mwaka jana, huku umaskini kwa wakazi waishio vijijini ikizidi kuwa mbaya.

Benki ya Dunia (WB) imebaini hayo kupitia utafiti wake ilioufanya Februari, mwaka huu, kuhusu hali ya siasa ya uchumi wa Tanzania, inayojulikana kama “Kutanua Mbawa Ukuaji wa Uchumi hadi Ustawi wa Pamoja”.

Akielezea utafiti huo, Mchumi Mkuu Afrika Mashariki na Kati, Jacques Morisset, alisema uchumi wa Tanzania umekua na kufika asilimia 6.5 kwa kipindi cha mwaka 2011/12 na kwa hiyo, imefanya vizuri kuliko nchi nyingine zinazoibuka kwa haraka kiuchumi, ikiwamo India na Brazil.

Hata hivyo, alisema licha ya kiwango kikubwa cha mfumuko wa bei usiopungua, kaya za vijiji, ambazo zina watu takriban theluthi mbili ya idadi ya watu wote nchini na asilimia 80 ya watu maskini, ambao wanaendelea kuishi katika mazingira magumu.

Mkurugenzi wa WB kwa nchi za Tanzania, Philippe Dongier, alisema ili kuondoa umaskini nchini, serikali inapaswa kusimamia nguvu kuu tatu, ambazo zina uwezo wa kuleta mageuzi hayo, ambazo ni kufanya mageuzi ya kilimo na kiwe cha kibiashara

Nyingine ni kupanua wigo wa biashara kuelekea bidhaa zenye thamani ya juu na kufanya shughuli nyingine mbali na kilimo, pamoja na uhamiaji kuelekea mijini.

Naibu Gavana wa Benki Kuu ya Tanzania (BoT), Natu Mwamba, alisema serikali katika miaka mitano ijayo, ina mpango wa kuboresha miundombinu iliyoko vijijini ili kurahisisha usafirishaji wa mazao kwenda mijini.

Alisema lengo kuu la serikali kwa sasa ni kuhakikisha uchumi wa nchi unakua kwa kasi kutoka asilimia 6.5 kwa mwaka huu hadi kufikia asilimia kubwa kufikia mwaka 2014.



 

CHANZO: NIPASHE